MASWALI YAULIZWAYO MARA NYINGI
- SHULE HII IMESAJILIWA?
Ndiyo. Usajili wa shule ulikamilika mwaka 1997. Namba ya usajili ni EM 10279. - MNATUMIA MIHTASARI GANI YA MASOMO?
Tunafuata mihtasari iliyotolewa na Wizara ya Elimu ya Tanzania kwa masomo yote. Pia tuna maelekezo mahususi katika kufundisha matumizi ya Maktaba. - JE, WANAFUNZI WENU HUFANYA MTIHANI WA KUMALIZA ELIMU YA MSINGI?
Ndiyo. Tumekuwa na wahitimu waliofanya mtihani wa serikali tangu mwaka 2001. - WANAFUNZI WENU HUFANYA MTIHANI KATIKA LUGHA YA KIINGEREZA?
Ndiyo. Wanafunzi wa shule zote zinazotumia Kiingereza katika mafunzo hufanya mtihani wa kumaliza elimu ya msingi kwa lugha ya Kiingereza. - JE, WANAFUNZI WENU HUCHAGULIWA KUENDELEA NA MASOMO YA SEKONDARI KATIKA SHULE ZA SERIKALI?
Ndiyo. Wanafunzi wanapata fursa sawa na wanafunzi walio katika shule za serikali. Pia wanaweza kuchagua kuendelea na masomo katika shule nyingi nzuri zisizo za serikali. - SHULE INA VIWANJA VYA MICHEZO?
Ndiyo. Tumetenga zaidi ya theluthi moja ya eneo la shule kwa ajili ya michezo. Kuna viwanja vya mpira wa kikapu na mpira wa wavu; pia lipo eneo la bembea. Tunatumia uwanja wa mpira wa miguu uliopo katika kambi ya jeshi jirani na shule yetu. - WANAFUNZI HUKAA WANGAPI DARASANI?
Kiwango cha juu kwa kila darasa ni wanafunzi thelathini, isipokuwa Shule ya Awali ambako idadi ya juu ni watoto ishirini tu katika kila mkondo. - WATOTO HUPEWA CHAKULA GANI?
Saa nne asubuhi watoto wanapata kikombe cha chai na mkate au andazi. Mlo wa mchana huwa na aina mbalimbali za vyakula kutoka siku moja hadi nyingine ikiwemo wali, pilau, nyama, maharage na kabichi. - RATIBA YA SIKU IKOJE?
Siku huanza saa moja na nusu asubuhi na kumalizika saa tisa na dakika ishirini mchana. Wanafunzi wa darasa la saba huondoka saa kumi na moja na nusu jioni Jumatatu hadi Ijumaa na saa kumi jioni siku ya Jumamosi. - MTOTO ANAWEZA KULETA CHAKULA SHULENI?
Hapana. Hairuhisiwi kuleta chakula, soda au juisi shuleni. Mpe mtoto maji safi na salama ya kunywa. - VIATU GANI VINARUHUSIWA?
Mtoto anatakiwa kuvaa viatu vyeusi vya ngozi na soksi nyeupe. Siku ya Ijumaa mtoto avae viatu vya michezo (raba). - WASICHANA WASUKE MTINDO GANI WA NYWELE?
Kama unapenda mwanao asuke nywele chagua mtindo wa kurudi nyuma tu maarufu kwa jina la “Utii wa Roda”.